Top Stories

UEFA, AFC na Concacaf waungana kupinga mpango wa FIFA

 

UEFA, AFC na Concacaf waungana kupinga mpango wa FIFA

Upinzani dhidi ya mpango wa FIFA wa kuruhusu wawekezaji binafsi kuingia katika shughuli za kibiashara za mashindano yake umeongezeka, baada ya UEFA, AFC na Concacaf kuweka wazi misimamo yao ya kuupinga.

FIFA inapendekeza kuanzisha kampuni ya FIFA Forward Enterprise (FFE) itakayoshughulikia shughuli za kibiashara za mashindano yake, huku wawekezaji wakiruhusiwa kununua hisa za wachache. Shirikisho hilo linaeleza kuwa hatua hiyo itasaidia kuongeza fedha za maendeleo ya soka duniani.

UEFA, inayowakilisha vyama 55 vya soka barani Ulaya, imesema haitashiriki mashindano ya FIFA ikiwa mpango huo utaendelea. Kwa upande wake, Concacaf yenye wanachama 41 imeeleza kuwa ina wasiwasi kuhusu mchakato uliotumika na ukosefu wa mashauriano ya kutosha kabla ya pendekezo hilo kutolewa.

Shirikisho la Soka la Asia (AFC), lenye wanachama 46, nalo limeungana na UEFA na Concacaf likisema mpango huo unahitaji kutafakariwa upya. AFC imeitaka FIFA kuboresha utaratibu wa mashauriano na kuhakikisha maamuzi makubwa yanashirikisha wadau wote wa mchezo.

Misimamo hiyo ya mabara matatu imeongeza shinikizo kwa FIFA wakati ikisaka uungwaji mkono wa wanachama wake 211 ili kupitisha pendekezo hilo. Hadi sasa, FIFA imeendelea kusisitiza kuwa mpango huo hauhusishi kuuza soka, bali unalenga kuongeza uwekezaji kwa maendeleo ya mchezo duniani.

Comments